top of page

Unatafuta mtoto? Jinsi ya kuongeza uwezekano wako ndani na nje ya chumba

Kuamua uko tayari kuanzisha familia ni hatua muhimu– na inayosisimua– katika maisha yako! Nivi iko hapa kukupa msaada kuipitia safari hiyo kwa kukushirikisha njia za kuongeza uwezekano wako wa kuwa na ujauzito, kama vile machaguo ya kiafya ya mtindo wa maisha, dondoo kwa ajili ya chumbani, na mambo ya uzushi kuhusu uzazi. Endelea kusoma kujifunza zaidi!


Dondoo za Mtindo wa Maisha Kuongeza Uwezo wa Kuzaa

Kujiandaa kwa ujauzito wenye afya huanza na kuwa na mtindo wa maisha wenye afya. Hivi hapa ndivyo vitu unavyoweza kufanya kubakia mwenye afya, aidha ukiwa unajaribu kuwa mjamzito au la:


Kuwa na uzito wa kiafya

Mwili wako utapitia mabadiliko makubwa wakati wa ujauzito. Hivyo kujijali mwenyewe kabla ya kujaribu kuwa na mtoto ni muhimu sana! Kuwa na malengo ya kuwa na uzito wa kiafya kunaweza kukusaidia kuwa mjamzito haraka zaidi wakati kukipunguza uwezekano wako wa kuwa na matatizo ya ujauzito. Ulaji wa kiafya na mazoezi ya mwili ya mara kwa mara yanaweza kukusaidia kudumisha uzito wa kiafya. Kwa mfano, kula matunda mengi, mboga za majani na nafaka, na kufanya matembezi mafupi ya kila siku kunaweza kukufanya mwenye afya. Kuwa makini usifanye mazoezi kupitiliza– kufanya mazoezi makali kwa zaidi ya masaa 5 kwa wiki kunaweza kupunguza uwezo wa kuzaa.


Usivute sigara, usinywe pombe nyingi, au kutumia madawa ya kulevya

Kuvuta sigara, pombe, na madawa ya kulevya vinaweza kupunguza uwezo wako wa kuzaa na kupelekea matatizo makubwa kwa mtoto wako, kama ujauzito kuharibika na ujauzito unaotunga nje ya mfuko wa uzazi. Wavutaji sigara mara nyingi wana viwango vidogo vya estrojeni, ambayo inaweza kuathiri mzunguko wako wa hedhi na kupunguza uwezekano wako wa kupata ujauzito. Vivyo hivyo kwa mwenzi wako, kuvuta sigara, kunywa pombe nyingi sana, na utumiaji wa madawa ya kulevya kunaweza kupunguza idadi ya mbegu za kiume na ubora wa mbegu za kiume kwa wanaume. Kumbuka, kama ukiwa mjamzito, hakuna kiasi cha pombe kilicho salama kunywa.


Zuia maambukizi ya magonjwa ya zinaa (STIs)

Baadhi ya maambukizi yanaweza kusababisha kutokuzaa kwa wanawake, kama vile klamidia na kisonono. Hivyo ni muhimu kutumia njia zuizi kama kondomu pindi ukiwa haujaribu kupata ujauzito.


Tumia Foliki Asidi kila siku

Kutumia foliki asidi (vitamini B) kunaweza kuboresha uwezekano wako wa kupata ujauzito kwa kuongeza upevushaji yai na kuchagiza urutubishaji yai. Pia humuweka mtoto wako mwenye afya pindi ukiwa mjamzito. Foliki asidi inapatikana kwenye vidonge vya vitamini vya prenatal, ambavyo unaweza kuvipata kutoka kwenye kliniki yako ya afya ya karibu. Habari njema ni kwamba baadhi ya vyakula vina foleti nyingi kiasilia, hivyo viongeze kwenye mlo wako! Hivi hapa ni vyakula baadhi ambavyo vina foleti nyingi:


  • Mboga za majani za kijani iliyokolea (figili, spinachi, chainizi, asparagus, Brussels sprouts, brokoli)

  • Maharage, karanga, na mbegu za alizeti

  • Matunda freshi na juisi za matunda

  • Nafaka

  • Ini

  • Vyakula vya baharini

  • Mayai

Punguza mkazo wako

Ikiwa una matatizo kwenye kupata ujauzito, inaweza kufadhahisha. Lakini kumbuka, kujali afya yako ya akili ni muhimu tu kama kuujali mwili wako. Hata kuchukua dakika chache tu kutilia mkazo kwenye pumzi yako kunaweza kuwa kitulizo. Shughuli kama yoga na kutafakari zinaweza pia kusaidia kupunguza mkazo wako.


Dondoo za chumbani kuongeza uwezo wa kuzaa

Ikiwa unajaribu kuwa mjamzito, ni muda wa kuacha kutumia uzazi wa mpango! Ni muda gani wa mapema zaidi utakuwa na uwezo wa kuzaa hutegemea kwenye njia gani ya uzazi wa mpango unayotumia. Kwa mfano, kama ukiacha kutumia njia ya uzazi wa mpango yenye vichocheo (kama vidonge), inaweza kuchukua mwezi kwa mzunguko wako wa hedhi wa kiasili kurudi kwenye hali ya kawaida. Ikiwa unatumia njia zuizi (kama kondomu), unaweza kupata ujauzito muda ujao usipoitumia.


Una uwezekano zaidi wa kuwa mjamzito kama unajamiiana mara kwa mara, lakini wakati ambao unajamiiana pia una umuhimu. Kuna siku chache kila mwezi ambapo una uwezekano zaidi wa kupata ujauzito, kutegemeana na mzunguko wako. Kwa mfano, kujamiiana kila siku 2 hadi 3 baada ya hedhi yako kuisha kunaweza kuongeza uwezekano wako wa kupata ujauzito. Unaweza pia ukatumia Njia ya Kalenda kuendelea kufuatilia siku zako za hatari (na zisizo hatari). Ikiwa Siku 1 ndio siku ya kwanza ya hedhi yako, Njia ya Kalenda inasema utakuwa kwenye siku za hatari zaidi kati ya siku za 8-19. Uwezekano wako wa kupata ujauzito utakuwa mkubwa zaidi ikiwa utajamiiana kwenye siku hizi!



Uzushi kuhusu Uwezo wa Kuzaa

Sasa hebu tuufichue baadhi ya uzushi kuhusu uwezo wa kuzaa!


Uzushi wa 1

Kutokuwa na uwezo wa kuzaa ni kosa la mwanamke

Sio kweli! Ujauzito uhitaji watu wawili…hivyo hiyo inamaanisha wote mwenzi wa kike NA wakiume lazima wawe na uwezo wa kuzaa.


Uzushi wa 2

Wanawake juu ya miaka 35 hawawezi kupata ujauzito

Hiyo inategemea. Uwezo wa kuzaa haupungui kutokana na umri, lakini bado inawezekana kwa wanawake wenye miaka zaidi ya 35 kupata ujauzito.

Wanawake wanaofikia kukoma hedhi hawawezi kupata ujauzito. Ukomo wa hedhi ni pindi hedhi yako inaposimama, ambao unaweza kutokea katika miaka yako ya 40 au 50.

Vizuri vipi kuhusu wanaume? Wanaume wana uwezo wa kutengeneza mbegu za kiume maisha yao yote, lakini ubora wa mbegu zao za kiume hupungua kutokana na umri. Wanawake na wanaume wengi hufikia uwezo mkubwa wa kuzaa wakiwa na miaka 30. Hiyo inamaanisha baada ya miaka 30, uwezo wa kuzaa kiasili unapungua kutokana na umri.


Uzushi wa 3

Uzazi wa mpango husababisha kukosa uwezo wa kuzaa

Sio kweli! Njia za uzazi wa mpango zenye vichocheo (kama vidonge) haziathiri uwezo wako wa kuwa na watoto baadae. Hata hivyo, maambukizi ya magonjwa ya zinaa yaani STIs yanaweza. Ndio maana ni wazo zuri kutumia njia ya uzazi wa mpango pamoja na njia zuizi (kama kondomu) kuzuia STIs na ujauzito. Pindi ukiwa unajaribu kutafuta mtoto, acha kutumia uzazi wa mpango. Vichocheo katika vidonge vya uzazi wa mpango hubakia ndani ya mwili wako kwa kipindi kifupi tu cha muda (ndio maana unavitumia kila siku). Hivyo pindi ukiacha kuvitumia, utarudi kwenye mzunguko wako wa kawaida na kuwa na uwezo wa kupata ujauzito ndani ya miezi michache.


Uzushi wa 4

Mikao fulani ya kujamiiana huongeza utungaji mimba

Unaweza ukawa umeshasikia mikao baadhi ni mizuri zaidi kwa ajili ya utungaji mimba. Hiyo sio kweli! Kitu cha muhimu zaidi ni kutafuta mkao ambao unahisi ni mzuri kwako na kwa mwenzi wako! Utungaji mimba ni pindi mbegu ya kiume ya mwanaume inakutana na yai la kike. Ili mradi mbegu ya kiume kutoka kwenye uume inaingia kwenye uke wakati wa kujamiiana, unaweza kupata ujauzito. Hivyo ziache kondomu kwenye droo!


Uzushi wa 5

Vipi kuhusu kulala chini baada ya kujamiiana?

Kulala chini baada ya kujamiiana hakutaongeza uwezekano wako wa kutunga mimba LAKINI kukumbatiana na mwenzi wako baada ya kujamiiana kuna faida nyingi kama…

  • Kutengeneza uhusiano imara zaidi

  • Usingizi mzuri zaidi

  • Kitulizo cha maumivu

  • Kupunguza hatari ya magonjwa ya moyo

  • NA mkazo mdogo zaidi


Uzushi wa 6

Afya ya ujumla haiathiri uwezo wa kuzaa

Sio kweli! Afya yako ya kimwili na kiakili ni muhimu sana. Kufanya machaguo ya kiafya ya mtindo wa maisha huboresha afya yako NA kuongeza uwezo wako wa kuzaa!


Kutokuwa na uwezo wa kuzaa

Kutokuwa na uwezo wa kuzaa ni nini? Tuseme unajaribu kutafuta mtoto. Unafanya ngono isio salama mara kwa mara lakini haupati ujauzito baada ya mwaka 1 wa kujaribu au zaidi. Hii inaitwa kutokuwa na uwezo wa kuzaa, na inaweza kuathiri wanaume na wanawake. Wenzi WOTE wawili lazima wawe na uwezo wa kuzaa ili mimba itunge.


Sababu za kutokuwa na uwezo wa kuzaa kwa wanawake:

☑ Hedhi zilizovurugika au kutokuwa na hedhi

☑ Historia ya mimba kuharibika zaidi ya mara moja

☑ Endometriosisi

☑ Historia ya maambukizi ya viungo vya uzazi vya mwanamke

☑ Dosari za vichocheo

☑ Dosari za vinasaba


Sababu za kutokuwa na uwezo wa kuzaa kwa wanaume:

☑ Historia ya kuumia korodani

☑ Historia ya kutokuwa na uwezo wa kuzaa na mwenzi mwingine

☑ Kupungukiwa nguvu za kiume, kama kudindisha au kuendelea kudindisha

☑ Dosari za vichocheo

☑ Dosari za vinasaba


Wakati wa kumuona daktari

Hizi hapa ni sababu baadhi kwanini unaweza kuhitaji kumuona mtaalamu wa afya:

☑ Umekuwa ukifanya ngono isio salama (hakuna kondomu, hakuna uzazi wa mpango) kwa zaidi ya mwaka 1

☑ Una miaka zaidi ya 35

☑ Ulikuwa na mimba iliyoharibika moja au zaidi

☑ Mwenzi wako ana shida kwenye kudindisha au kuendelea kudindisha

☑ Haupati hedhi, unapata hedhi zilizovurugika, au unatokwa damu nyingi

☑ Wewe au mwenzi wako alikuwa na maambukizi ya magonjwa ya zinaa (STIs)

☑ Una tatizo la kiafya la muda mrefu kama kisukari au shinikizo la juu la damu



Kuna sababu nyingi kwanini unaweza kuwa na shida kupata ujauzito NA pia kuna masuluhisho mengi! Kwenda kwenye kituo cha huduma za afya, ofisi ya daktari, au kliniki kunaweza kukusaidia kupata majibu unayohitaji.


Kumbuka, ikiwa una shida kwenye kupata ujauzito, kamwe sio kosa lako. Hata kama haupati dalili hizi, bado ni wazo zuri kupata uchunguzi wa afya wa mara kwa mara: kabla, wakati wa, na baada ya ujauzito. Nivi iko hapa kukusaidia katika mchakato mzima.

 

Una maswali kuhusu kujamiiana, maambukizi ya magonjwa ya zinaa yaani STIs, na uzazi wa mpango? Kumbuka unaweza kuchati na Nivi kwenye WhatsApp na Facebook Messenger muda wowote. Ni mazungumzo binafsi, ya usiri, na bure!


bottom of page